CUF yamataka Nahodha ajizuru

Monday 30 May 2011

IDADI YA WATU WALIOSOMA HABARI HII: counter
*Ni kutokana na mauaji ya wananchi  watano Tarime
*Yalaani, yasema huo ni ukiukwaji wa haki za binadamu


Na Agnes Mwaijega

BARAZA Kuu la Chama cha Wananchi (CUF) limemtaka Waziri wa Mambo ya Ndani kuwajibika kutokana na mauaji yaliyotokea wilayani Tarime
lakini pia kufanyika kwa uchunguzi wa kina juu ya tukio hilo.

Hatua hiyo ilifikiwa Dar es Salaam jana na Mwenyekiti wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mapendekezo mbalimbali yaliyoazimiwa na kikao cha baraza hilo.

Alisema kuwa baraza hilo linalaani vitendo vya ukiukaji na uvunjaji wa haki za binadamu hususan mauaji ya raia yanayofanywa na Jeshi la Polisi ambayo yamekuwa yakiripotiwa kila mara.

"Inatuumiza sana kwa kuwa inaonekana jambo hili ni la kawaida kwa sababu watendaji wake hawachukuliwi hatua yoyote," alisema.

Prof. Lipumba alisema kuwa baraza hilo pia linamtaka Rais Jakaya Kikwete kutambua kuwa jukumu la kuleta maendeleo ya Watanzania ni la watu wote hivyo serikali yake isisite kutumia sera mbadala za CUF kwa maendeleo ya taifa.

Alisema serikali kupitia wizara ya Fedha na Uchumi na Wizara ya Nishati na Madini inatakiwa kuchukua hatua za kuhakikisha nchi na wananchi wake wananufaika na rasilimali za madini zilizopo hapa nchini hususani madini ya dhahabu ambayo bei yake katika soko la dunia imepanda.

"Dhahabu inayouzwa nje ni dola bilioni 1.5 kwa mwaka sawa na  asilimia 40  ya bidhaa za Tanzania zinazouzwa nje ya nchi," alisema.

Alisisitiza kuwa baraza hilo linataka kuona utajiri wa nchi unawanufaisha wananchi na kuisaidia nchi kujikomboa kutoka katika dimbwi la umasikini na kuacha kutegemea misaada kutoka nje ambayo imeifanya nchi kuwa tegemezi kwa miaka mingi.

Aliongeza kuwa baraza hilo linamtaka Waziri wa Nishati na Madini Bw.William Ngeleja kujiuzulu kwa kuwa ameshindwa kutumia vyanzo vya umeme vilivyopo nchini ili kukabiliana na tatizo sugu la nishati linaloikumba nchi yetu kwa sasa.

Alisema nchi imejaliwa vyanzo vingi ya umeme na maeneo mengi ya maporomoko ya maji,makaa ya mawe ,madini na hata umeme wa jua ambao hauna gharama kubwa ya kufua.

"Ni miaka 50 tangu tupate uhuru hatuna sababu yoyote  ya kutokuwa na umeme wa uhakika, ni ufisadi tu ambao umekithiri katika serikali yetu," alisema.

0 comments:

Post a Comment